Kamati ya kudumu ya bunge ya nishati na madini imeiagiza wizara ya nishati kupeleka umeme haraka kwenye mgodi mkubwa wa uchimbaji dhahabu unaomilikiwa na serikali wa Stamigold uliopo mkoani Kagera ili kuunusuru mgodi huo kujiendesha kwa hasara kutokana na kutumia shilingi milioni mia saba kwa kila mwezi kununua mafuta ya dizeli kuendeshea mgodi huo
Akizungumza katika ukaguzi wa mgodi huo mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe.Raphael Chegeni akiambatana na wabunge anasema mgodi huo unajiendesha kwa hasara kutokana na kutumia mamilioni ya fedha za walipa kodi kuendeshea mitambo ya uchimbaji na uchakataji wa dhahabu hali inayotishia mgodi huo kufilisika na kufungwa.
Waziri wa madini Mhe.Dotto Biteko anasema mgodi huo unasuasua katika uzalishaji kutokana kukabiliwa na changamoto lukuki ikiwepo ubadhilifu uliotokea kwa uongozi uliopita pamoja na ukosefu wa mtaji wa uendeshaji wa shughuli za uchimbaji.
Mwenyekiti wa bodi ya Stamico nchini Meja Jenerali Michael Isamuhyo anasema kupatikana kwa umeme kutoka gridi ya taifa kutapunguzia mgodi huo kujiendesha kwa hasara pamoja na kuongeza uzalishaji huku wajumbe wakiitaka bodi mpya kuhakikisha mgodi unawanufaisha wananchi wanaowazunguka maeneo hayo.