Back to top

Naibu waziri Kanyasu atoa masharti kwa wenye leseni za kuchimba madini

16 September 2019
Share

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu amewataka wananchi wenye leseni za kuchimba madini ndani ya Hifadhi za Misitu, mapori ya Akiba pamoja na Hifadhi za Taifa  wafuate sheria zinazotakiwa kabla ya kuanza kazi ya machimbo.

Amewaeleza wananchi hao  licha ya kuwa wana leseni inayowaruhusu kuchimba madini ndani ya Hifadhi wanachotakiwa ni  kuomba vibali kutoka kwenye Taasisi husika za  Uhifadhi.

Mhe.Kanyasu amefafanua kuwa kuingia ndani ya Hifadhi na kuanza kuchimba madini bila kuwa na vibali kutoka kwa Taasisi husika ya uhifadhi  ni kosa kisheria na endapo watakutwa watakamatwa na sheria itafuata mkondo wako

Ametoa msimamo  huo jana mkoani leo Geita  wakati akizungumza  kwenye mkutano wa hadhara na wakazi wa eneo la Mgusu  ambao shughuli yao kuu ya kiuchumi ni Uchimbaji wa madini ya Dhahabu.

Kufuatia hali hiyo Mhe.Kanyasu amewataka Wananchi wenye leseni za kuchimba madini ndani ya Hifadhi ya msitu unaosimamiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania 
(TFS) katika eneo hilo la Mgusu  waombe kibali kutoka TFS ili waendelee na shughuli za machimbo bila kubugudhiwa.


Amesema  kumekuwa na mazoea kwa  wananchi  mwenye leseni za kuchimba madini ndani ya Hifadhi kufikiri kuwa Kwa vile wana leseni hiyo basi  wana haki ya  kuanza kuchimba madini   bila ya kuwa na   kibali kutoka TFS.

Kanyasu amewaeleza wananchi hao  kuwa  inapotokea ardhi ina madini kunakuwa na  umiliki wa aina mbili, kunakuwa na umiliki wa  leseni ya juu ya ardhi na leseni ya chini ya ardhi, hivyo mwenye leseni ya chini ya ardhi akitaka kuchimba madini chini ya ardhi  anatakiwa aombe kibali kwa mwenye leseni ya juu ya ardhi ambapo katika eneo hilo wenye ardhi ya juu ni TFS.

Hivyo amewataka wananchi hao kama wanataka kuanza kuchimba madini ndani ya  msitu huo   waombe kibali kutoka TFS kwa sababu kwa mujibu wa sheria TFS ndio yenye leseni ya umiliki wa juu ya ardhi.

Amesema wakikubaliana na TFS watapewa  utaratibu wa kulipa kiasi fulani cha pesa pamoja kuonesha mpango wa kurudishia miti mara baada ya shughuli za uchimbaji madini utakapomalizika 

Aidha, Mhe. Kanyasu amewataka wananchi wa eneo hilo waache tabia ya kukata miti kwa ajili ya shughuli za madini pasipo kuomba kibali kutoka TFS

''Tutakayemkamata akifanya uharibifu ndani ya Hifadhi ya misitu huo, tutahakikisha analipa gharama zote za miti atakayokamatwa nayo'' alisisitiza Mhe. Kanyasu.