Watu watano wakazi wa Msamala wilayani Songea mkoani Ruvuma wamenusurika kufa baada ya nyumba yao kuungua moto na sehemu kubwa ya samani za ndani kuungua moto.
Mmiliki wa nyumba iliyoungua moto bw. Albano Nyandindi anasema moto huo ulitokana na hitilafu ya umeme na ulitokea wakati akiwa sebuleni na familia yake ya watu watano na wakati mlipuko wa moto unatokea walikimbia nje kuita majirani waliosaidia kuzima moto wakati wakisubiri askari wa zimamoto na watu wa TANESCO waliofika baadaye.
Wananchi waliosaidia kuzima moto wanasema tukio hilo lilileta taharuki kubwa kwa familia iliyounguliwa na nyumba kutokana na moshi mwingi uliokuwepo ndani ya nyumba hiyo huku pia wakilalamikia tabia ya tanesco mkoa wa ruvuma kukata umeme bila taarifa.
Viongozi wa TANESCO na zimamoto mkoa wa Ruvuma walipotafutwa wazungumzie tukio hilo wameshindwa kupatikana kutokana na kuwa katika mapumziko ya sikukuu ya pasaka huku askari wa zimamoto walioshiriki kuzima moto wakishindwa kuzungumza kwa madai kuwa wao si wasemaji.