Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Magufuli ametangaza amehamia rasmi makao makuu ya nchi Dodoma ambapo amesema tayari viongozi wote wamekwishahamia makao makuu ya nchi Dodoma huku akiwataka wananchi kuendelea kujitokeza kujiandikisha katika daftari la uchaguzi wa serikali za mitaa na kuchagua viongozi watakaokwenda na kasi ya serikali ya awamu ya tano
Rais Dkt.Magufuli ameyasema hayo wakati akijiandikisha katika daftari la uchaguzi wa serikali za mitaa katika kijiji cha Chamwino Ikulu yalipo makazi yake ikiwa ni muda mfupi mara baada ya kuwasili akitokea katika ziara yake mkoani Katavi ambapo mara baada ya kujiandikisha akazungumza na wakazi wa kijiji hicho na kutangaza rasmi kuhamia makao makuu ya nchi Dodoma.
Wakizungumza mara baada ya zoezi la kujiandikisha baadhi ya wakazi wa kijiji cha Chamwino Ikulu wametumia nafasi hiyo kumshukuru Mhe.rais Dkt.Magufuli kwa kuhamia rasmi Dodoma ambapo pia wameeleza changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo changamoto ya uhaba wa maji katika kijiji hicho
Akijibu changamoto za wananchi hao ia rais Dkt.Magufuli amesema atahakikisha changamoto zinazowakabili wananchi hao zinaisha katika kipindi hiki ambacho tayari amehamia katika Ikulu ya Chamwino Dodoma ambapo amewataka wananchi kuendelea kuunga mkono serikali ya awamu ya tano