Serikali imekataa kutoa kibali kwa mgodi mkubwa wa uchimbaji madini ya dhahabu wa Geita Gold Minning (GGM) kuendesha uchimbaji wa madini chini kwa chini kutokana na mgodi huo kushindwa kutekeleza maagizo kumi yaliyotolewa na serikali ikiwemo agizo la kuwalipa fidia wananchi zaidi ya mia tatu ambao nyumba zao ziliharibiwa vibaya na milipuko ya baruti kwa zaidi ya miaka kumi.
Akizungumza mara baada ya kukagua utekelezwaji wa maagizo ya serikali katika mgodi huo waziri wa madini Mheshimiwa Dotto Biteko ameagiza kuundwa tume maalumu ikihusisha (TAKUKURU) kushughulikia madai ya wanainchi juu ya fidia za nyumba zao ili kumaliza malalamiko ya muda mrefu.
Mkuu wa mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel anasema malalamiko ya fidia kwa wananchi ambao nyumba zao ziliharibiwa na milipuko na zingine kuwekewa vigingi ni ya muda mrefu na kuundwa kwa tume hiyo kutamaliza kilio cha wananchi
Akizungumzia maagizo ya serikali kwa niaba ya mkurugenzi mkuu wa GGM makamu wa rais wa mgodi huo Simon Shayo anasema wamepokea maagizo ya serikali na wamejipanga kuziondoa changamoto za fidia kwa wananchi ambao hawajalipwa madai yao.