Back to top

SAMIA MGENI RASMI KILELE MIAKA 60 YA JESHI LA POLISI.

16 September 2024
Share

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi  Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Mh.  Dk. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika Kilele cha Miaka 60 ya Jeshi la Polisi inayofanyika katika shule ya Polisi Tanzania Moshi Mkoani Kilimanjaro Septemba 17, 2024.
 
Akitoa taarifa hiyo Moshi Mkoani Kilimanjaro, Msemaji wa Jeshi la Polisi Nchini, Naibu Kamishna wa Polisi, DCP David Misime, amesema kuwa awali Jeshi hilo lilitoa taarifa kuhusiana na maadhimisho ya miaka 60 ya Jeshi la Polisi Tanzania nakufanyika shughuli mbalimbali katika Mikoa na vikosi vya Jeshi hilo hapa nchini.
 
DCP Misime ameongeza kuwa shughuli hizo ni pamoja nakupima afya wananchi bure katika Hosptali Kuu ya Jeshi hilo iliyopo Barabara ya kilwa (kilwa Road) Jijini Dar es Salaam na Zahanati zote za Jeshi zilizopo Mikoa yote.
 
Sambamba na hilo amebainisha kuwa mambo mengine yaliyofanyika katika maadhimisho hayo ni Pamoja na Jeshi la Polisi kushirikiana na Jamii katika michezo Pamoja na kutoa elimu juu ya kutoa taarifa za wahalifu na uhalifu katika mikoa mbalimbali hapa nchini.
 
Vilevile ameweka wazi kuwa ulifanyika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Maafisa wakuu waandamizi wa Jeshi la Polisi ambao umemalizika siku ya Jana Septemba 15,2024 huku akibainisha kuwa Septemba 17,2024 Jeshi hilo linatarajia kuhitimisha kilele cha maadhimisho hayo katika Shule ya Polisi Tanzania Moshi Mkoani Kilimanjaro.
 
Pia amesisitiza kuwa maadhimisho hayo yataambatana na tuzo na zawadi kwa askari ambao wamelitumikia Jeshi la Polisi kabla na baada ya uhuru huku akiweka wazi kuwa maandalizi yamekamilika na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Daktari Samia Suluhu Hassan.