Back to top

TRA JENGENI MAHUSIANO MAZURI NA WAFANYABIASHARA KAVUU

04 May 2024
Share

 Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe.Geophrey Pinda ameitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kujenga mahusiano mazuri na wafanyabiashara wa eneo Majimoto katika Halmasauri ya Mpimbwe Wilaya ya Mlele mkoa wa Katavi.

Mhe. Pinda ametoa kauli hiyo wakati wa kikao cha pamoja kati ya Maafisa wa TRA Makao makuu na wafanyabiashara wa eneo la Majimoto kilichofanyika katika Halmashauri ya Mpimbwe.

Kikao hicho cha siku moja kinafuatia kuwepo malalamiko kutoka kwa wafanyabiashara kuwa wamekuwa wakibugudhiwa na maofisa wa TRA katika eneo hilo jambo walilolieleza kuwa limekuwa likisababisha usumbufu katika biashara zao.

Mhe.Pinda ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kavuu, amesema, ni wajibu wake kuhakikisha maisha ya wafanyabiashara katika eneo la Majimoto yanakuwa rafiki na kusisitiza kuwa, eneo hilo linapoteza wateja wengi.

Aidha, Mhe, Pinda amewataka maafisa wa TRA katika eneo hilo kutokuwa na dharau kwa wafanyabiashara na kuhoji unapomdharau mlipa kodi unategemea kitu gani huku akisisitiza mamlaka hiyo kutoa huduma nzuri kwa kwa wateja.

Kwa mujibu wa Mbunge huyo wa jimbo la Kavuu, Mamlaka ya Mapato Tanzania lazima maafisa wake wawe rafiki na wafanyabiashara ili kuondoa vikwazo vinavyoweza kupeleka mkwamo kwa wafanyabiashara.

Amebainisha kuwa, TRA pamoja na mambo mengine lazima ijikite kutoa elimu kwa mlipa kodi kama ambavyo maafisa wake walivyofanya kwa kwenda kwa wafanyabiashara wa Majimoto huku akiwataka maafisa hao kuacha kabisa siasa katika shughuli za kibiashara. ‘’Nasema haya ili mje na mageuzi makubwa kwa lengo la kuboresha’’. Amesema Mhe, Pinda

Kwa upande wake Mkurugenzi wa halmashauri ya Mpimbwe Bi.Shamim Daud amesema, zaidi ya asilimia hamsini ya mzunguko wa fedha katika halmashauri yake inatoka eneo la Majimoto na ndiyo maana halmashauri yake imeweka uwekezaji mkubwa katika eneo hilo ili kuhakikisha huduma za jamii zinaimarishwa na kupunguza changamoto kwa watu wanaoingia na kutoka eneo hilo.