Back to top

SERIKALI, SEKTA BINAFSI KUIMARISHA HUDUMA ZA FEDHA NCHINI

25 February 2025
Share

Serikali imekuwa ikihimiza taasisi za fedha kuipeperusha bendera ya Tanzania nje ya nchi kwa kufanya uwekezaji wa kimkakati. Hayo yameelezwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko, Kahama mkoani Shinyanga wakati akizindua tawi la Benki ya Exim.

“ Kahama ni kitovu kikubwa cha shughuli za kiuchumi, hasa sekta ya madini ambayo inachangia kwa kiasi kikubwa kwenye pato la Taifa. Zaidi ya madini, mji huu pia ni maarufu katika sekta ya kilimo na biashara. Ni wazi kuwa ufanisi wa sekta hizi unategemea upatikanaji wa huduma za kifedha imara na zinazokidhi mahitaji ya wajasiriamali na wafanyabiashara,” amesema Dkt. Biteko.

Ameendelea “Hivyo, kwa kufungua tawi hili, Exim Benki inatoa fursa ya kipekee kwa wakazi wa Kahama kupata huduma za kifedha zinazoendana na shughuli zao za kiuchumi. Na kunaleta manufaa makubwa kwa jamii ya hapa Kahama, kwa wateja wengine wa benki na benki yenyewe kwa ujumla,”

Dkt. Biteko ametaja manufaa hayo kuwa ni kuongezeka kwa fursa za uchumi kwa kuongeza ajira, kuongeza mapato ya benki na hivyo kutumia sehemu ya faida yake kuchangia maendeleo ya jamii ikiwemo kusaidia makundi maalum kadhaa yenye uhitaji yaani (Corporate Social Responsibility - CSR) 

Aidha, manufaa mengine ni kuongezeka kwa mapato ya kodi Serikalini na kuongezeka kwa ushindani wa huduma za kibenki.

Pia, Dkt. Biteko ameipongeza benki hiyo kwa hatua kubwa na kwa jitihada zake za kuleta huduma za kifedha karibu zaidi na wananchi pamoja na kuiwakilisha Tanzania  katika nchi za Comoros, Uganda, Djibouti, pamoja na Ethiopia.

Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko ameipongeza Benki ya Exim kwa kuisaidia jamii kupitia Exim Cares “ Nimefurahi kusikia kuwa kabla ya kuzindua wa tawi hili tayari mmechangia vifaa vya matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama vyenye gharama ya zaidi ya shilingi milioni 25. Mchango huo wa vifaa vya matibabu utasaidia kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa Kahama. Hatua kama hizi zinaonesha mshikamano wa sekta binafsi na Serikali katika kuboresha ustawi wa wananchi.”
 
Pia, amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kuimarisha huduma za kifedha na kuhakikisha kuwa zinapatikana kwa urahisi na kwa ufanisi kwa kila Mtanzania.

Vilevile, Dkt. Biteko ametoa wito kwa Benki hiyo kuwashika mkono na kuwakuza vyema wananchi wa kawaida na wa hali ya chini ambao wao watakuwa ni wateja muhimu. Aidha, uchumi wa wananchi hao wa kawaida hukuwa kwa kasi kutokana na shughuli zao za kiuchumi na hivyo kuisaidia pia benki kukua.

Benki hiyo ya Exim inatarajiwa kuwasaidia wananchi wa Kahama wanaohitaji huduma za kibenki ili kukua kiuchumi kwa kutoa huduma mbalimbali kama vile fursa za kufungua akaunti, kupata mikopo, na kufanikisha malipo mbalimbali kwa njia salama na rahisi zaidi.

“ Niwatoe wasiwasi Benki ya Exim  kuwa Kahama inafedha na inaendelea kukuwa kwa sababu ya uwepo wa bandari kavu na katika sekta ya madini mfano Kabanga nikeli na bidii ya watu wa hapa ya kufanya kazi. Hapa ni soko kubwa na muone fahari watu wa Kahama wanatajirika kupitia benki yenu,” amemalizia Dkt. Biteko.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Anamringi Macha amesema kuwa ufunguzi wa tawi la benki hiyo ni kielelezo kuwa shughuli za uchumi ni nyingi na zitaendelea kuimarishwa.

Ameongeza kuwa Mkoa huo una matawi ya benki 11 ambayo yote pia yapo Kahama hivyo  ni kiashiria kuwa Kahama ipo kibiashara na kuwa Mkoa huo uko tayari kushirikiana na benki hiyo.