Back to top

ONGEZEKO LA THAMANI YA MAUZO KATI YA TANZANIA NA INDONESIA IMEONGEZEKA

03 September 2024
Share

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema uhusiano wa kibiashara baina ya Tanzania na Indonesia, umekuwa maradufu ikizingatiwa ongezeko la thamani ya mauzo ya nje kutoka Tanzania, kwenda Indonesia kwa wastani wa dola za Marekani milioni 13.53 mwaka 2019 hadi dola milioni 33.77 mwaka 2023.

Bidhaa kuu za Tanzania zinazouzwa nchini Indonesia ni pamoja na Tumbaku, Kakao, Maharage, Karanga, Karafuu, Pamba, na Mafuta ya Mawese.

Rais Dk. Mwinyi amebainisha kuwa Tanzania na Indonesia, zinaadhimisha miaka 60 ya uhusiano wa kidiplomasia kwa mwaka huu 2024, kwani ni jambo la fahari kwa nchi hizo mbili kujivunia urafiki uliodumu na unaoendelea kukua siku hadi siku.

Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo katika mwendelezo wa siku ya pili ya Jukwaa la Indonesia na Afrika 2024, uliofanyika katika ukumbi wa mikutano, hoteli ya Mulia, Bali, Indonesia.

Dk. Mwinyi katika jukwaa hilo amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Tanzania bado ina fursa nyingi za uwekezaji ikiwemo kilimo, madini, utalii, na uchimbaji wa mafuta na gesi na uchumi wa buluu hivyo, Rais Dk. Mwinyi amewakaribisha wawekezaji kutoka Indonesia kuja Tanzania Bara na Zanzibar kuzifanyia kazi fursa hizo.

Kwa upande wa elimu, Rais Dk. Mwinyi ameishukuru Serikali ya Indonesia kwa kuendelea kuiunga mkono Tanzania katika sekta ya maendeleo ya rasilimali watu kupitia udhamini wa masomo ya muda mfupi na muda mrefu katika nyanja mbalimbali.

Rais Dk. Mwinyi ameishawishi Serikali ya Indonesia iongeze udhamini wa masomo pamoja na kubadilishana uzoefu katika maeneo mbalimbali kama vile huduma za Afya na Sayansi ya Tiba, Uhandisi, ICT, Uvuvi, Utalii, Ufugaji wa Samaki, na Kilimo.

Wakati huo huo Rais Dk. Mwinyi ameshuhudia utiaji saini (MoU) wa Makubaliano ya udhibiti wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi kwa lengo la ushirikiano katika usajili wa bidhaa hizo, ukaguzi pamoja na kupeana taarifa za madhara ya dawa na vifaa tiba kwenye masoko.