Back to top

UGONJWA WA FMD WAJADILIWA KUTOVUKA MIPAKA YA NCHI ZA EAC NA SADC

10 September 2024
Share

Wataalamu kutoka Sekta ya Mifugo katika Jumuiya za Afrika Mashariki (EAC) na Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) wamekutana kwa ajili ya kujadili namna ya kudhibiti ugonjwa wa miguu na midomo (FMD) unaoshambulia mifugo ili usivuke mipaka ya nchi.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw. Abdul Mhinte akizungumza mara baada ya kufungua mkutano huo, jijini Dar es Salaam, amesema lengo la mkutano huo ni kuhakikisha ugonjwa huo unadhibitiwa kwa kuwa nchi za jumuiya ya EAC na SADC zina mahusiano ya karibu.

Bw. Mhinte ameongeza kuwa Tanzania inajumuika katika jumuiya zote mbili na kwamba imekuwa mwenyeji wa mkutano huo kwa ajili ya kudhibiti ugonjwa huo ambao umekuwa ukivuka mipaka kutoka nchi moja kwenda nyingine.

“Mkutano huu umehusisha Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), wataalamu wanakutana kwa ajili ya kujadili ugonjwa huo ili usivuke kwenda nchi moja kwenda nyingine kwa kuwa jumuiya hizo zina mahusiano ya karibu.” Amebainisha Bw. Mhinte.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) nchini Tanzania, Bi. Nyabenyi Tipo amesema takwimu ya Mwaka 2013 ugonjwa wa FMD umekuwa na madhara makubwa ya kiuchumi na kusababisha hasara ya Dola za Kimarekani (USD) Milioni 11.

Bi. Tipo ameongeza kuwa takriban watu Milioni 700 kote duniani wanategemea Sekta ya Mifugo katika kuendesha maisha yao na kwamba ugonjwa huo umekuwa ukipunguza uzalishaji wa mifugo pamoja na ukuaji wa soko la biashara kwa mifugo na mazao ya mifugo.

Naye Mwakilishi wa Shirika la Afya ya Wanyama Duniania (WOAH), Kanda ya Afrika Mashariki Bw. Neo Mapitse amewaomba washiriki wa mkutano huo kwamba kila kitakachojadiliwa lazima kitoe matokeo chanya na endelevu ili kufikia malengo waliyojiwekea katika kudhibiti ugonjwa wa FMD.

 Ameongeza kuwa ni wakati wa kuimarisha jitihada za kudhibiti ugonjwa huo kuhakikisha afya na ustawi wa mifugo pamoja na jamii kwa kuondoa mapungufu ambayo hayajafanyiwa kazi na kuwa wazi katika kuyafanyia kazi ili kutoa matokeo chanya.

Aidha, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo nchini kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Benezeth Lutege amewaarifu washiriki wa mkutano huo kuwa katika Mwaka wa Fedha 2024/2025 serikali inatarajia kufanya kampeni ya chanjo na utambuzi wa mifugo dhidi ya magonjwa ya homa ya mapafu ya ng’ombe, sotoka ya mbuzi na kondoo pamoja na mdondo.

Pia, amesema kampeni hiyo yenye kugharimu fedha za kitanzania zaidi ya Shilingi Bilioni 28 ni moja ya mikakati ya serikali katika kudhibiti magonjwa ya mifugo kwa kuweka vipaumbele kwenye kudhibiti magonjwa hayo na kuwa na mifugo inayokidhi soko la kitaifa na kimataifa.

Mkutano wa kujadili namna ya kudhibiti ugonjwa wa miguu na midomo (FMD) unaoshambulia mifugo unafanyika hapa nchini kwa siku tatu ambapo unajumuisha wataalamu wa Sekta ya Mifugo kutoka Jumuiya za Afrika Mashariki (EAC) na Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), ili ugonjwa huo usivuke mipaka ya nchi za jumuiya hizo.