Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, ameiagiza Kamati ya Ulinzi na Usalama wilaya ya Kigoma Ujiji kufanya uchunguzi na kuchukua hatua baada ya kubaini harufu ya ufisadi katika ujenzi wa vyumba vya madarasa 9 ya shule ya msingi Kigoma yanayojengwa kwa ufadhili wa Serikali ya Japan kwa gharama ya shilingi milioni 200.
Dkt. Kijaji ametoa maelekezo hayo baada ya Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Dkt. John Tlatlaa, kueleza kwamba mradi huo unahusisha ujenzi wa vyumba 10 vya madarasa na vyoo vyenye matundu 12, wakati mkataba ulioingiwa kati ya Manispaa hiyo na Mkandarasi inayoonesha kwamba yatajengwa madarasa 9 na vyoo vyenye matundu 12.
Baada ya mjadala kati yake na Kaimu Mkurugenzi huyo wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, akamwelekeza Kaimu Mkuu wa Wilaya hiyo Bi. Mwanamvua Mrindoko kuchukua hatua za kiuchunguzi.